Na.Kitengo cha Habari na Mawasiliano Serikalini(W) Masasi.
Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Masasi Mkoani Mtwara leo tarehe 19/06/2025 limevunjwa rasmi huku wakimtaka Mkurugenzi Mtendaji Ndg.Alphaxad Etanga pamoja na Watendaji wake wote kuwa makini kwenye suala zima la Mapato ili kufikia lengo la Halmashauri la kukusanya zaidi ya shilingi bilioni kumi kwa Mwaka.
Madiwani hao pia wamewataka watendaji na Wataalamu kwa ujumla kuhakikisha wanasimamia vizuri ile asilimia 10 ya mapato ya ndani waliyoipanga inapelekwa kwenye Miradi ya Afya.
Maagizo hayo yametolewa kwenye Mkutano maalumu wa Baraza la mwisho la Madiwani ambalo lilianza mnamo mwaka 2020 na kuhitimishwa leo juni 19,2025.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Masasi Ndg.Alphaxard Etanga akisoma taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Maendeleo katika kipindi cha Miaka mitano (2020/21 -2024/25) pamoja na mapendekezo ya uendeshaji wa shughuli za Halmashauri kipindi cha Mpito, amesema katika kipindi cha miaka 5 baraza limepata mafanikio makubwa ambapo jumla ya shule mpya saba (7) za msingi zimejengwa na kusajiliwa na kufanya jumla ya shule 137 kutoka shule 130 zilizokuwepo mwaka 2020/2021.
Amesema kwa hatua hiyo takwimu za uandikishaji wa darasa la awali zimepanda kutoka Wanafunzi 6395 hadi 6745 sawa na ongezeko la 5% huku elimu msingi uandikishaji umeongezeka kutoka 7835 hadi 8464 sawa na asilimia 8% ya uandikishaji.
"Kwa Sekta ya elimu Sekondari shule za Serikali zimeongezeka kutoka shule 27 hadi kufikia shule 37 zenye usajili na hii ikiwa ni ongezeko la asilimia 10 na kufanya kila kata katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi kuwa na shule za Sekondari,kwaiyo haya ni mafanikio makubwa yanayotokana na usimamizi wenu Madiwani " alisisitiza Ndg.Etanga
Akizungumzia sekta ya Afya Mkurugenzi huyo amefafanua kuwa kwa kipindi cha Miaka mitano hali ya upatikanaji wa Dawa katika Hospitali ya Wilaya, Vituo vya afya na Zahanati imeongezeka kutoka asilimia 88% hadi 96% sawa na ongezeko la asilimia 8%.
"Kwa kiupekee nimshukuru sana Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea fedha nyingi ambazo zimeleta tija kubwa kwa jamii ya wana Masasi Katika kipindi cha Miaka mitano "
Sambamba na hilo Halmashauri kwa kutambua mchango mkubwa walioutoa viongozi hao imetoa vyeti vya pongezi kwa Madiwani wa kata zote 34 pamoja na wabunge wa jimbo la Ndanda na Lulindi.
19/06/2025
Masasi - Bomani
Anuani ya Posta: S.L.P 60 Masasi
Simu ya mezani: 023-2510031
Simu ya kiganjani: 023-2510031
Baruapepe za Watumishi: ded@masasidc.go.tz
Hakimiliki @2017 Halmashauri ya Wilaya ya Masasi. Haki Zote Zimehifadhiwa